Thursday 16 June 2016

Watoto na Vijana Wa Ariel Camp Wafanya Utalii Mkoani Kilimanjaro,Washuhudia Ziwa Chala Lenye Miujiza Mingi

1



Ni siku ya tatu,Jumatano Juni 15,2016 ambapo watoto na vijana 50 kutoka mikoa ya Shinyanga na Simiyu wapo mkoani Kilimanjaro katika kambi ya siku tano iliyoandaliwa na shirika la Ariel Glaser Pediatric Aids Healthcare Initiative (AGPAHI) linalojihusisha na mapambano dhidi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi katika mikoa ya Shinyanga,Simiyu na Geita.




Siku ya kwanza na ya pili watoto na vijana walijifunza masomo mbalimbali katika ukumbi wa Lutheran Uhuru Hotel mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.Siku ya tatu ikawa ni kwa ajili ya kufanya utalii wa ndani katika maeneo yenye vivutio ili kujifunza mambo mbalimbali na kuongeza uelewa wao.



Watoto na vijana hao walitembelea kituo cha  Kiutamaduni kinachohusika na kilimo cha Kahawa cha "Kilimani Cultural Tourism Enterprise -Kahawa Shambani", kilichopo katika kata ya Uru Kaskazini, halmashauri ya wilaya ya Moshi Vijijini ambalo ni maarufu kwa utalii wa kahawa na mila za kabila la Kichaga.

Eneo jingine walilotembelea ni mpaka wa nchi ya Tanzania na Kenya uliopo  Holili mkoani Kilimanjaro.

Utalii wao uliishia katika Ziwa Chala lililopo kijiji cha Malowa ya wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro.

Ziwa hilo (pichani juu) lilitokana na mlipuko wa Volkano miaka kadhaa iliyopita katika eneo alilokuwa anaishi mzee maarufu kwa jina la "Mzee Chala" aliyekufa kwa kuzama ardhini pamoja na mali zake zote ikiwemo mifugo yake wakati wa mlipuko huo.

Ziwa Chala linatajwa kuwa la miujiza ambapo kila mwaka watu wasiopungua  watatu hupoteza maisha na pia  hutokea miujiza ya kutisha kila mwisho wa mwaka.

Mwandishi wetu Kadama Malunde alikuwepo katika ziara hiyo ya utalii,anatusimulia kwa njia ya picha kuanzia mwanzo mpaka mwisho.Tazama hapa chini
Eneo la Kwanza la Utalii:Ofisi ya Kituo cha Kiutamaduni cha Wakulima wa Kahawa katika kata ya Uru Kaskazini.Kituo hicho kimezungukwa na mashamba ya kahawa ya wakulima kutoka vijiji vya  Ngari,Mlawi,Ongoma na Msuni ambao hujihusisha na kilimo cha kahawa aina ya Arabica.Wakulima hao wanalima kahawa kwa njia ya asili.

Washiriki wa Ariel Camp wakiwasili eneo "Kilimani Cultural Tourism Enterprise -Kahawa Shambani"



Mmoja wa wakulima wa kahawa, mzee Jerome Kessy akiwakaribisha watoto na vijana,maafisa kutoka AGPAHI na walezi waliokuwa katika ziara hiyo. Eneo hilo "Kilimani Cultural Tourism Enterprise -Kahawa Shambani" limekuwa kivutio kwa watu wengi na watalii wanaofika mkoani humo.
Kila aliyefika "Kilimani Cultural Tourism Enterprise -Kahawa Shambani",alipata kikombe cha kahawa ili kuonja utamu wa kahawa ya asili inayolimwa na wakulima wa Kata ya Uru Kaskazini. Kushoto ni mzee Denis Shiyo,ambaye ni mmoja wa wakulima wa eneo hilo akitoa maelekezo wakati wa kunywa kahawa.Kulia niAfisa miradi huduma unganishi kwa jamii AGPAHI, Richard Kambarangwe akiwamiminia kahawa watoto na vijana
Mzee Denis Shiyo,ambaye ni mmoja wa wakulima katika eneo hilo akibadilishana mawazo na vijana na watoto hao kabla ya kuwapeleka mashambani ili kujionea jinsi kilimo cha kahawa kinavyofanyika.



Mzee Shiyo akizungumza na vijana kuhusu kilimo cha kahawa kabla ya kwenda shambani



Safari ya kuelekea mashambani ikaanza..vijana na watoto wakagawanywa katika makundi manne,kila kundi na mkulima mmoja.Kushoto ni mmoja wa wakulima wa kahawa akiwa na vijana.


Wapiga picha nao hawakuwa nyuma...



Kundi hili wakaona vyema kupiga picha kwanza kabla ya kuingia kwenye mashamba
Maafisa kutoka AGPAHI wakiteta jambo wakati wakielekea kwenye mashamba ya kahawa
Tunaelekea mashambani...
Walezi wa watoto, vijana na maafisa kutoka AGPAHI wakielekea kwenye mashamba ya kahawa.
Mkulima Jerome Kessy (kulia) akiwaeleza vijana jinsi zao la kahawa lilivyoletwa na wakoloni  ambapo mpaka sasa wananchi wameendelea kujihusisha na kilimo cha zao hilo.
Vijana wakielekea mashambani



Mashamba na familia za wakulima zipo kwenye milima...hivyo vijana hao walilazimika kupanda milima 






Hapa ni katika familia ya mkulima wa zao la kahawa bwana Modest Faustine Ngoli katika kitongoji cha Tawingo, kijiji cha Msuni, kata ya Uru Kaskazini. Kulia ni mzee Kessy akielezea jinsi kilimo cha kahawa kinavyofanyika. Alisema mbegu ya kahawa inaota kati ya siku 55 hadi 60 tangu kuwekwa ardhini kupata kitalu,kisha kitalu kinahamishiwa shambani na inachukua takribani miaka mitatu ndiyo mti wa kahawa kutoa maua na kahawa kuchumwa.

Mashine inayotumika kubangua kahawa
Mkulima wa zao la kahawa Modest Faustine Ngoli akiweka maji kwenye mashine inayotumika kubangua kahawa


Mkulima Jerome Kessy akionesha mbegu ya kahawa iliyokaushwa

Kushoto ni mwandishi wa habari wa Malunde1 blog,bwana Kadama Malunde akifanya mahojiano na mkulima wa zao la kahawa Modest Faustine Ngoli katika kitongoji cha Tawingo kijiji cha Msuni kata ya Uru Kaskazini. Ngoli alisema miongoni mwa changamoto wanazokabiliana nazo kuwa ni gharama kubwa ya dawa za kutibu zao la kahawa

Eneo la pili la Utalii-Hapa ni katika ofisi za Uhamiaji mpaka wa Tanzania na Kenya katika eneo la Holili.Pichani ni Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji katika mpaka wa Tanzania na Kenya bwana Kagimbo Hosea Alphonce akiwakaribisha watoto na vijana. Katika ofisi hizi watoto na vijana walijifunza mambo mbalimbali yanayotakiwa kuzingatiwa pale mtu anapohitaji/anapotaka kusafiri kutoka nchi moja kwenda nyingine.

Bwana Alphonce alisema wanajihusisha shughuli zote zinazohusu watu wanaotoka Tanzania kwenda Kenyana wanaotoka Kenya kwenda Tanzania.

Bwana Alphonce akiwaongoza watoto,vijana na walezi na maafisa wa AGPAHI kwenye jengo la uhamiaji ambapo ndani kuna wafanyakazi wa nchi ya Tanzania na Kenya.
Watoto,vijana,walezi na maafisa wa AGPAHI wakiingia kwenye jengo la uhamiaji la mpaka wa Kenya na Tanzania.
Watoto na vijana wakiingia ndani ya jengo hilo

Eneo la mapokezi katika jengo la uhamiaji ambapo ukaguzi kwa kila anayeingia hufanyika.



Bwana Alphonce akitoa maelezo kwa vijana na watoto.



Mmoja wa afisa wa mamlaka ya mapato Tanzania waliopo katika jengo hilo la uhamiaji akitoa maelezo namna wanavyofanya kazi.
Tunasikiliza maelezo....
Eneo la tatu la utalii:Hapa ni katika Ziwa Chala lililopo katika Kijiji cha Malowa wilayani Rombo mkoani Kilimanjaro. Ziwa hili lilitokana na mlipuko wa Volkano miaka kadhaa iliyopita. Jina la ziwa Chala lilitokana na mzee maarufu 'Chala', ambaye alifariki kwa kudidimia na mifugo yake ardhini baada ya kutokea mlipuko wa volkano.

Wakazi wa eneo hilo wanasema ni ziwa la ajabu na lenye miujiza mingi ambapo kila mwaka watu wasiopungua watatu hupoteza maisha na kila mwisho wa mwaka wazee wa kimila hufanya matambiko yao katika ziwa hilo.Wanaamini kuwa ndani ya ziwa kuna Chunusi wanaosababisha vifo vya watu.




Watoto na vijana wakiwa  Campsite ya Ziwa Chala, eneo ambalo limejengwa na mwekezaji binafsi ambapo watalii hufika na kuangalia ziwa kwa uzuri zaidi. Ziwa hilo ni miongoni mwa vivutio mkoani Kilimanjaro ambapo robo ya ziwa iko Kenya na robo tatu iko Tanzania.


Mwongoza watalii katika Campsite ya  Ziwa Chala, bwana Ali Saluwa akielezea historia ya Ziwa hilo la ajabu. Alisema kina cha ziwa hilo ni kuanzia mita 90 hadi 300 na halina ufukwe,ukiteleza na ukawa hujui kuogelea ni rahisi kupoteza maisha.


Bwana Saluwa alisema ziwa hilo lina mikondo miwili chini (kuingiza na kutoa maji) hivyo maji ya ziwa hilo huwa hayapungui wala kuongezeka kwani linapokea maji kutoka mlima Kilimanjaro wakati wa kiangazi kisha kupeleka maji hayo Ziwa Jipe lililopo eneo la Upareni mkoani Kilimanjaro.

Bwana Saluwa akielezea kuhusu miujiza ambayo hutokea kila mwisho wa mwaka katika ziwa hilo ambapo alisema mwezi Desemba hutokea upepo mkali wa aina yake,mashua zisizokuwa na watu zikipita ndani ya ziwa na sauti za ajabu ajabu zikitawala.


Muonekano wa Ziwa Chala,ni ziwa la ajabu halina ufukwe na maji yake ni safi kabisa kwa kunywa. Ndani ya ziwa kuna samaki aina ya Tilapia na hakuna mamba.



Bwana Saluwa akiendelea kueleza maajabu ya Ziwa Chala ambalo limeua wazungu wengi waliofika hapo kufanya utafiti pia baadhi ya watanzania waliofika kuvua samaki,kutalii na hata kuogelea bila kufuata maelekezo.


Sehemu ya ziwa Chala,upande unaouona mbele yako ni nchi ya Kenya.

2